Pages

Ads 468x60px

LIKE THIS PAGE FIRST.

Friday, February 8, 2019

Ofisi Ya Rais-Utumishi Yafanya Ufuatiliaji Wa Utekelezaji Wa Waraka Wa Mavazi Kwa Watumishi Wake


Idara ya Ukuzaji  Maadili, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kushirikiana na Kamati ya Uadilifu ya ofisi hiyo, imefanya ufuatiliaji wa Utekelezaji wa Waraka wa Mavazi Na. 3 wa Mwaka 2007 kwa watumishi wa ofisi hiyo kwa lengo la kujiridhisha na kiwango cha utekelezaji wake, ikiwa ni pamoja na kuhimiza watumishi wa umma nchini kuzingatia waraka huo mahala pa kazi.

Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Ukuzaji Maadili, Sehemu ya Ufuatiliaji Uzingatiaji wa Maadili, Bibi Janeth Mishinga mara baada ya kukamilika kwa zoezi la ufuatiliaji wa Utekelezaji wa Waraka huo kwa watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambao unawaelekeza watumishi wa umma aina ya mavazi wanayostahili kuyavaa mahala pa kazi.

Bibi Mishinga amesema, Ofisi ya Rais-Utumishi ni msimamizi wa miongozo mbalimbali ya kiutumishi ikiwemo Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma ambapo kanuni ya kwanza inaelekeza utoaji wa huduma bora na kuongeza kuwa moja ya kigezo cha watumishi wa umma kutoa huduma bora ni pamoja na kuvaa mavazi  yenye staha.

Bibi Mishinga amefafanua kuwa, zoezi hilo la ukaguzi katika ofisi ya Rais-Utumishi limebaini kuwa asilimia 95 ya watumishi wameonekana kutekeleza vema waraka huo wa mavazi ikiwemo kuwahi kazini na asilimia tano ya watumishi waliobainika kutotekeleza waraka huo wamekumbushwa kuuzingatia.

Aidha, Bibi Mishinga ametoa wito kwa wasimamizi wa taasisi zote za umma nchini  kufanya ufuatiliaji wa utekelezaji wa waraka huo na kuwahimiza watumishi walio chini yao  kuwahi kazini kwa ili kutoa huduma bora na kwa wakati kama ambavyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli anavyohimiza.

Bibi Mishinga  amesisitiza kuwa, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora  ikiwa ndio msimamizi wa waraka huo wa mavazi itaendelea kufanya ukaguzi na ufuatiliaji  katika taasisi zote za umma nchini na haitosita kuwachukulia hatua za kinidhamu watumishi wote wa umma watakaobainika kuukiuka.

No comments:

Post a Comment