Pages

Ads 468x60px

LIKE THIS PAGE FIRST.

Saturday, March 1, 2014

IKULU YAKANUSHA NYONGEZA YA POSHO


RAIS Jakaya Kikwete hajaongeza posho kwa wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kutoka Sh 300,000 za sasa na kueleza kuwa hajawahi kupokea maombi ya nyongeza ya posho hiyo.
Badala yake amefanya marekebisho ya mpangilio wa posho hizo ambapo itabaki Sh 300,000 hiyo hiyo ya awali.

Maelezo hayo ya Rais Kikwete yaliyotolewa kupitia kwa Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu, Salva Rweyemamu yanabainisha kuwa maombi kutoka katika bunge hilo aliyopokea ni kufanyia marekebisho mpangilio kwa posho hiyo na amekubali na kuruhusu kufanya kama wajumbe walivyoomba.
“Kilichoombwa si nyongeza ya posho bali ni ile Sh 300,000 kupanga katika mpangilio tofauti na awali,” alisema.
Katika mpangilio wa awali katika posho ya Sh 300,000 ilikuwa posho ya kujikimu Sh 80,000 na Sh 220,000 posho maalum ya kuhudhuria vikao.
Katika posho hiyo ya kuhudhuria vikao iligawanywa posho ya dereva kati ya Sh 40,000 na Sh 45,000 kwa siku, usafiri wa ndani yaani mafuta au teksi, mawasiliano na matumizi mengine binafsi.Mchanganuo mpya haukutolewa na Ikulu.
Mgawanyo huo uliopitishwa na Rais uliwasilishwa kwake na Kamati ya Kushughulikia Posho iliyoundwa na Mwenyekiti wa Muda wa Bunge hilo, Pandu Ameir Kificho.
Kamati hiyo ilikuwa na wajumbe sita nao ni William Lukuvi, Mohamed Abood Mohamed, Freeman Mbowe, Paul Kimiti, Jenister Mhagama na Asha Bakari.
Kamati hiyo iliyoanza kazi Februari 19 iliongozwa na mambo manne likiwamo la uhalisia wa gharama za maisha mjini Dodoma na aina ya wajumbe walioteuliwa kwa kuainisha pato lao kabla ya kuwa wajumbe wa Bunge.

Pia sheria kuhusu taratibu za posho, uwazi wa posho zinavyotolewa na ulinganisho wa malipo ya kuzingatia aina za wajumbe. Kamati baada ya kujiridhisha iliwasilisha mapendekezo yake kwenye mamlaka hiyo, ili itafakari mapendekezo hayo na kutoa maelekezo.
Rweyemamu alieleza msimamo huo wa Rais kuhusu posho kutokana na kauli iliyotolewa juzi na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Mkoa wa Dodoma kusema iwapo wajumbe hao wataongezwa posho na mamlaka za uteuzi watafanya maandamano ya amani nchi nzima.

Aidha kumekuwapo na taarifa kuwa posho hiyo imeongezwa na kufika Sh 500,000.
“Mamlaka ya uteuzi haiwezi kuongeza posho kutokana na kuwa haijawahi kupokea maombi ya ongezeko la posho hiyo na wala haijaongeza posho hiyo kama ilivyoelezwa katika baadhi ya vyombo vya habari,” alisema Rweyemamu.
Chimbuko la hoja Februari 19 ikiwa ni siku ya pili ya kikao cha Bunge Maalumu, Richard Ndassa Mbunge wa Sumve, ndiye aliibua suala hilo la posho akisema Sh 300,000 kwa siku wanayolipwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba ni ndogo.
Pia alidai wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wameongezwa posho na SMZ jambo ambalo linaleta tofauti bungeni lakini baadaye Katibu wa Baraza la Wawakilishi, Yahya Khamis Hamad, alikiri wawakilishi walidai nyongeza hiyo ya posho lakini SMZ haikuwajibu.
Wawakilishi hao walidai wanapokuwa nje ya SMZ wanalipwa Sh 200,000 hivyo baada ya kufika kwenye Bunge Maalumu na kubaini posho ya kujikimu ni Sh 80,000, waliwasilisha maombi waongezwe kiasi kinachopungua, ambacho ni Sh 120,000 kwa siku.
Akiungwa mkono na Mbunge wa Kishapu, Suleiman Nchambi, walihoji sababu za wao kupewa posho hiyo wakati wajumbe wa Tume ya Marekebisho ya Katiba walilipwa Sh 500,000 walipokuwa wakikusanya maoni.

Kwa mujibu wa wanaotaka nyongeza, mchanganuo wa matumizi yao ni kwamba hadhi ya hoteli wanayopaswa kulala ni ya kuanzia Sh 70,000. Pia wanahitaji mafuta ya gari, kulipa madereva na kutoa fedha kwa watu mbalimbali wanaowaomba msaada.
Kutokana na madai hayo ya wajumbe ya nyongeza ya posho kulizuka malalamiko kutoka kwa watu mbalimbali wanaopinga nyongeza hiyo kwa madai iliyopo ni kubwa na wengine wanasema inatosha.
Miongoni mwa waliopinga hadharani nyongeza hiyo kutoka ndani ya bunge hilo ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini Kabwe Zitto, Julius Mtatiro, Mbunge wa Karatu Israel Natse, Naibu Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba na Mbunge wa Nkasi Mohamed Kessy.

No comments:

Post a Comment